Recent

FAQ's

Powered by Blogger.

Facebook

Technology

Business

Gadgets

Search This Blog

Blog Archive

Videos

Technology

Sports

Fashion

Business

Header Ads

Social

Contact Form

Name

Email *

Message *

Categories

Advertise Here

Tags

Nature

Comments

Popular

Popular Posts

Jose Chameleone anunua pair ya kiatu yenye thamani ya Milioni 25 za kitanzania

Written By Bizzi on Monday, April 17, 2017 | April 17, 2017

Ile tabia ya watu maarufu kununua vitu vyenye thamani imeendelea kuongezeka kwa kasi hivi sasa, ambapo Jose chameleone mwanamziki anayetokea UGANDA ametrend kwa kuonyesha viatu vyake viwili vyenye thamani ya dola za kimarekani 12,500.

Jose chameleone amesema kununua viatu hivyo hamaanishi kwamba anajionyesha ila ni moja ya njia anayotumia kumshukuru Mungu.

Jose Chameleone akiwa amevishika viatu hivyo
Jose ni mmoja kati ya wanamuziki wenye mafanikio zaidi kwa wakati huu, ambapo utajiri wake amekuwa akiuweka wazi mara kwa mara kwa kuonyesha magari na nyumba anzozimiliki.

Wavuta bangi wapata kanisa lao,litafunguliwa siku ya bangi duniani April 20


Wapenzi wa bangi na kuabudu wamepata kanisa lao, kanisa hili lipo mjini Denver Marekani na litafunguliwa April 20 ikiwa ni siku ya wavutaji duniani.
Taasisi ya dini Elevation Ministries imetangaza uzinduzi wa kanisa hili la kimataifa International Church of Cannabis, ikiwa ni sehemu ya wavutaji kujiskia huru kuabudu.

Waumini wa kanisa hili wanajiita Elevationists, na Jengo la kanisa hili linamiaka 113 na limerekibishwa hivi karibui…

2 Chainz amesha kubali kufanya show kwenye uzinduzi wa kanisa hili.

Forbes yatoa orodha ya wasanii wapya wanaoingiza mkwanja mrefu zaidi 2017


Forbes imeachia orodha mpya ya wasanii wapaya wanaoingiza mkwanja mrefu zaidi “Forbes Hip-Hop Cash Princes”
Kwenye Oorodha hiyo wapo Bryson Tiller ambaye alikuwa akiingiza $100,000 kwa usiku mmoja kwenye tour yake ya muziki huku akiingiza nyimbo mbeli zilioongoza kwenye chart ya Top 40 na album yake ya TrapSoul ikiwa imeenda Platnum,Desiigner mbali ya nomination ya Tuzo za Grammy, Ngoma yake ya Pandaimeongoza chart nyingi ikiwemo Billboard Hot 100 na pia emepata dili nono la kusainiwa kwenye lebel ya Kanye West G.O.OD Music.

Hii ndio orodha kamili,
Desiigner
D.R.A.M.
Tory Lanez
Lil Uzi Vert
Lil Yachty
Noname
Isaiah Rashad
Stormzy
Bryson Tiller
Young M.A.

Mwaka jana Boi-1da, DeJ Loaf, Fetty Wap, G-Eazy, Joey Bada$$, Lil Dicky, Logic, na Metro Boomin walitajwa kwenye orodha hiyo.

Hawa ndio Waigizaji 20 wa filamu wanaolipwa zaidi duniani

Forbes wametoa orodha mpya ya waigizaji wa filamu wa kiume wanaolipwa fedha zaidi duniani.

Dwayne ‘The Rock’ Johnson ndiye ameongoza orodha hiyo Lakini pia kwenye orodha hiyo kuna waigizaji wa kiwanda cha filamu cha Bollywood,

20. Harrison Ford – $15m
19. Matthew McConaughey – $18m
18. Amitabh Bachchan – $20m
17. Will Smith $20.5m
16. Chris Pratt $26m
15. Leonardo Dicaprio $27m
14. Salman Khan – $28.5
13. Mark Wahlberg $30m
12. Adam Sandler $30m
11. Brad Pitt – $31.5m
10. Akshay Khumar $31.5m
9. Robert Downey Jr – $33m
8. Shah Rukh Khan – $33m
7. Vin Diesel – $35m
6. Ben Affleck – $43m
5. Johnny Deep – $48m
4. Tom Cruise – $53m
3. Matt Damon – $55m
2. Jackie Chan – $61m
1. Dwayne ‘The Rock’ Johnson $64m

Hii ndio listi mpya ya matajiri 10 duniani iliyotolewa na Forbes


Jarida linalofatilia maisha ya watu maarufu na mali zao “Forbes” limetoa list ya watu matajiri zaidi duniani, na wakati huu kuna mabadiliko makubwa ya watu waliofanikiwa kuingia kwenye Top 10. Bilionea Bill Gates ameendelea kushika nafasi ya kwanza ikiwa ni mara ya 18 kati ya 23 zilizowahi kutajwa.

Kijana mfanyabiashara wa mitandao Mark Zuckerberg ambaye ni mmiliki wa mitandao maarufu ya kijamii kama Facebook, Whatsapp na Instagram amepanda mpaka nafasi ya 5 mwaka huu.

Hii ndio listi nzima ya matajiri wa dunia.

Aliyekuwa kiongozi wa Freemason Tanzania, Sir Andy Chande afariki dunia


Aliyekuwa kiongozi wa Jumuiya ya Freemason Afrika Mashariki, Sir Jayantilal Keshavji ‘Andy’ Chande amefariki Dunia.

Sir Andy Chande alikuwa mwanachama wa Freemason kwa takribani miongo 6 tangu ajiunge. Alizaliwa Mombasa, Kenya Mei 7, 1928 ingawa wazazi wake walikuwa wakiishi Bukene Mjini, Mkoani Tabora,Tanzania.

Jeshi la Polisi limewaua majambazi waliowaua askari 8 Kibiti


Jeshi la Polisi Tanzania limesema limewaua majambazi wanne ambao walikuwa ni sehemu ya kundi la majambazi lililowashambulia na kuwaua askari 8 wilayani Kibiti mkoani Pwani jana usiku.

Akizungumza na wanahabari leo, Kamishna wa Oparesheni na Mafunzo wa jeshi hilo, Nsato Marijani amesema kuwa mara baada ya kundi hilo kuwashambulia askari, kikosi kingine cha askari kilifanya msako na kubaini maficho ya majambazi hao.

Amesema baada ya kuwabaini, yalifanyika mashambulizi ya kurushiana risasi, ambapo majambazi wanne waliuawa pamoja na kukamata bunduki 4 zikiwemo SMG mbili zilibainika kuwa kati ya zile zilizoporwa na majambazi hao.

Akielezea tukio hilo lilivyokuwa, Kamishna Marijani amesema kundi la waharifu walikuwa na silaha za moto na ambao idadi yao haikujulikana liliweka mtego na kufanikiwa kuishambulia kwa risasi gari iliyokuwa na askari 9 waliokuwa wakitoka katika malindo kurudi kambini, na kuwaua askari 8 kati yao huku mmoja akijeruhiwa mkononi.

Amewataja askari waliuawa kuwa ni pamoja na Mkaguzi Msaidizi Peter Kiguu, Koplo Francis, PC Haruna, PC Jackson, PC Zakaria, PC Siwale, PC Maswi na PC Ayoub, ambapo pia walipora bunduki 7 zikiwemo SMG 4.

Kufuatia tukio hilo, Kamishna Marijani ametangaza vita na waharifu wote katika maeneo hayo, ambapo amesema vyombo vya ulinzi na usalama vinaanza oparesheni maalum katika mkoa wa Pwani, kuhakikisha vinawasaka na kukomesha mauaji hayo ikiwa ni pamoja na kuwachukulia hatua.

Polisi anayedaiwa kumuua mwenzake asakwa kwa dau

“Mpaka sasa jeshi limekwisha poteza skari zaidi ya 10, inatosha…. Tunakwenda kwenye oparesheni maalum, hatutakuwa na mzaha, tutawasaka popote walipo na kuwashughulikia kikamilifu, ,,, watajua tofauti ya moto na maji… mpaka jana idadi ilikuwa ni 8 kwa nne, lakini nawahakikishia kuwa ndani ya wiki moja idadi hiyo itakuwa imebadilika, na tutakuwa na hesabu tofati” amesema Marijani

Kuhusu hofu ya ugaidi, Kamishna Marijani amesema tukio hilo siyo la kigaidi bali ni uhalifu wa kawaida, huku akibainisha kuwa Tanzania hakuna ugaidi

Katika hatua nyingine, jeshi hilo limepiga marufuku uendeshaji wa pikipiki katika maeneo yote ya Kibiti, Mkuranga na Rufiji zaidi ya saa 12:00 jioni. Amesema usafiri wa boda boda utaruhusiwa kati ya saa 12:00 asubuhi hadi saa 12:00 jioni

Kampuni ya Uber kutengeneza magari yanayopaa


Muhandisi wa zamani wa shirika la maswala ya angani Nasa ameajiriwa na kampuni ya teksi Uber kusaidia katika utafiti wake wa kutengeza magari yanayoruka.

Mark Moore anajiunga na Uber kama mkurugenzi wa uhandisi wa angani.

Lengo la Uber katika kutengeza magari yanayoruka lilianza mwezi Oktoba ambapo maswala ya kupaa na kutua yalijadiliwa.

Uber tayari inawekeza katika magari ya kujiendesha ikishirikiana na kampuni ya Volvo na Daimler.

Katika mipango yake Uber imesema kuwa katika mahitaji ya angani ,kampuni hiyo ina uwezo wa kuimarisha uchukuzi wa mijini na kuwapunguzia wateja wake muda wanaopoteza kila siku wanaposafiri.

Mpango huo utashirikisha mtandao wa ndege za kielektroniki ambazo zitapaa na kushuka wima.

Moore alisema mpango kama huo katika jarida lililochapishwa wakati alipokuwa Nasa.

Alisema kuwa mpango wa kutengeza vitu vinavyopaa kielektroniki ni mpango muhimu wa kiteknolojia wa ndege na kuongezea kwamba kitu kinachozuia kuanza kwa mpango huo ni betri zitakazotumika.

Kampuni ya kutengeza magari ya ya Aeromobil kutoka nchini Slovakia ni miongoni mwa kampuni ambazo zina mpango wa kutengeza gari la kuruka ambayo inatarajiwa kuingia katika soko mwaka huu.

YAJUE MAMBO 11 KUHUSU IKULU YA MAREKANI(WHITE HOUSE)

Kuna mambo mengi usiyoyajua kuhusu ikulu ya marekani ambayo pengine kwa msomaji anaweza kushangazwa akiyajua.Hivyo katika kusherehekea Sikukuu ya Rais baadhi ya watu waliweza kutoa mambo 11 kuhusu ikulu ya Marekani ambayo ina jumla ya vyumba 132 na imejengwa katika eneo la ukubwa wa mita za mraba 17,000. Mambo hayo ni haya yafuatayo:

Awali ilijulikana tu kama jengo la West Wing ni ofisi za watendaji. West Wing ilijengwa na Rais Teddy Roosevelt akiwa na lengo la kutenganisha makazi na sehemu za ofisi. Hata hivyo alipoingia madarakani Rais Taft akaamua kuunganisha jengo la ofisi la West Wing na majengo ya makazi akisema anataka kuhusika zaidi na shughuli zzote za White House.

Ndani ya ikulu ya Marekani kuna nyumba pacha ambapo inaelezwa kuwa James Hoban ni mbunifu na raia wa Ireland alichora kwa mfano wa jengo la Leinster la jijini Dublin huko Ireland. Awali jengo la Leinster lilikuwa makazi ya kiongozi wa Leinster na kwa sasa ni jengo la bunge la Ireland. Kwa maneno mengine White House ya Marekani inashabihiana na jengo la bunge la Ireland.

Katika ikulu ya marekani hakuna kitu kama chakula cha bure, hata kwa Familia ya rais wa nchi hiyo.Mwishoni mwa kila mwezi, Rais anapata bili yake binafsi ya kulipia chakula chake na familia yake ikiwa ni pamoja na huduma zote zinazotolewa ndani kama kufanya usafi, dawa ya meno, na vifaa vya vyoo, ambayo hukatwa kutoka katika mshahara wake dola 400,000 kila mwaka.

Watu wengi wanajua kuhusu eneo la Bowling lakini kuna mambo mengine kadhaa ya kuvutia katika eneo la chini ya White House. Ukiachilia chumba cha ‘situation’ ambacho hutumiwa na rais wa Marekani pindi kunapotokea dharura ya kitaifa au kimataifa kuna vitu kama duka la maua, karakana ya mafundi seremala, na ofisi ya daktari wa meno kiasi kwamba rais hana sababu ya kutoka nje ya White House kwa shida yoyote ile. Kila kitu kimo ndani ya ikulu ya Marekani.

Ikulu ya marekani imekuwa ya kushangaza kwa kuwa moja ya taasisi maarufu duniani. White House kila wiki inapata hadi wageni 30,000 na barua 65,000. Aidha karibu simu 3,500 hupigwa, barua pepe 100,000, na faksi 1000 hupokelewa katika ikulu hiyo ya Marekani kwa wiki.

Pamoja na ukweli kuwa Ikulu ya marekani hairuhusu kuingilia faragha za Raisi pamoja na familia yake ambao hutumia simu maalumu bado huwezi kuweka hakikisho la mia kwa mia kuwa baadhi ya mazungumzo ndani ya ikulu ya Marekani huvuja.

Ikulu ya marekani ilijengwa kwa msaada wa watu wengi. wasanii wengi wa Ulaya na wafanyakazi wahamiaji ikiwa ni pamoja na waashi kutoka Scotland. Matofali na plasta ilifanywa na wafanyakazi kutoka Ireland na Italia. Katika hali ya kusikitisha historia za kumbukumbu za mishahara zinaonyesha wajenzi wengine walikuwa watumwa wamerekani wenye asili ya Afrika.

Jina la White House halikuwa likitumiwa hapo kabla hadi alipoingia madarakani rais Theodore Roosevelt ndipo ikulu hiyo ikapewa jina hilo. Awali ikulu hiyo ilijulikana kama kasri la watendaji.


Kama ilivyo kwa majengo yoyote makubwa duniani, mauzauza hayakosekani na miongoni mwa mauzauza hayo kubwa ni lile la rais Winston Churchill kukataa kulala tena katika master bedroom ya Lincoln baada ya mzimu wa Lincoln kumtokea rais Churchill ambapo alimwona ameketi kando ya tanuru chumbani alipotokeza kutoka kuoga.

White House daima imekuwa katika mabadiliko ambapo awali haikutarajiwa kuchaguliwa kwa rais mlemavu na ilipotokea ilibidi kurekebisha milango na kujengwa kwa lifti ili kumwezesha rais mlemavu kutembelea maeneo yote ya ikulu ikiwa ni pamoja na kujengwa kwa bwawa maalumu la matibabu kwa rais huyo mlemavu.

Katika ajabu la kumi na moja rais Clinton alifanya marekebisho ya ikulu ya aina yake. Yeye alijenga baseni la kuogea lenye maji moto lenye ukubwa wa kutosha watu saba. Pia kulikuwa na uwezekano wa watu wawili tu kutumia beseni hilo.

Mke wa Roma Mkatoliki Afunguka Tena


Mke wa msanii Roma Mkatoliki Nancy Mshana (kushoto) akiwa na mume wake.

Mke wa msanii Roma Mkatoliki Nancy Mshana amefunguka kwa mara ya kwanza toka mume wake alipotekwa na kupatikana na kuwashukuru Watanzania ambao walikuwa pamoja na yeye katika kipindi kigumu.

Nancy ametumia maneno ya kwenye Biblia kutoka katika kitabu cha Yeremia kufikisha ujumbe wake kwa watu ambao wamemfanyia ubaya mume wake na kusema kuwa na wao watakutwa na mabaya hayo.

“(Yeremia 30:16-17) Basi, watu wote wakulao wataliwa; na adui zako wote watakwenda kufungwa; kila mmoja wao; na hao waliokuteka nyara watatekwa; na wote waliokuwinda nitawafanya kuwa mawindo. Maana nitakurudishia afya, nami nitakuponya jeraha zako, asema Bwana .Ameen” Alinukuu mke wa Roma Mkatoliki

Mbali na hilo Nancy alitumia nafasi hiyo kuwashukuru wote ambao wamesimama na wao katika kipindi hiki kigumu.

“Ahsanteni wote mliosimama na sisi katika kipindi kigumu tulichopitia !! Mungu awabariki sana” aliandika Nancy

Msanii Roma Mkatoliki bado anaendelea na matibabu kufuatia tukio lake la kutekwa na kuumizwa katika sehemu mbalimbali za mwili wake.

KASHFA ZAZIDI KUMWANDAMA ZUMA PRETORIA, AFRIKA KUSINI

CHAMA cha upinzani cha Congress of the People (Cope) kinapanga kumshitaki Rais Jacob Zuma kwa kumpatia ulinzi maalumu kwa viongozi wa ngazi za juu (VIP) aliyekuwa Mwenyekiti wa Tume ya Umoja wa Afrika, Nkosazana Dlamini-Zuma.

Dk. Dlamini-Zuma alipewa ulinzi wa VIP kufuatia madai ya kutishiwa maisha, ambayo polisi walikuwa wakiyachunguza.

Mwingine atakayehusishwa katika kesi hiyo ni Waziri mpya wa Polisi, Fikile Mbalula.

Cope ilieleza hatua hiyo ni matumizi mabaya ya fedha za walipa kodi na ni haramu na kinyume cha Katiba.

“Dk. Dlamini-Zuma si mgombea urais wala mbunge anayestahili kupewa ulinzi wa VIP ambao ni maalumu kwa maofisa waandamizi wa serikali na wakuu wa mataifa wa kigeni na wake zao,” kiongozi wa Cope Mosiuoa Lekota, alisema katika taarifa.

Alisema analaani vikali vitendo vya ukiukaji sheria na Katiba vinavyofanywa na Rais Zuma na Mbalula.

“Zuma na Mbalula wanapaswa kufikishwa mahakamani kueleza sababu ya matumizi haya mabaya ya fedha za walipa kodi ‚” alisema Lekota.

Kauli ya Lekota imekuja baada ya Jeshi la Polisi kufichua Zuma aliyetangaza nia ya kuwania urais wa Chama tawala cha Africa National Congress (ANC) na ambaye ni mke wa zamani wa Rais Zuma aliendelea kupokea ulinzi wa VIP kutokana na uchunguzi unaoendelea kuhusu vitisho vilivyoelekezwa kwake.

Msemaji wa Jeshi la Taifa la Polisi Sally de Beer alikiri kuwapo kwa ulinzi wa ziada.

Lakini Meja Jenerali De Beer alikataa kueleza kiundani kuhusu aina ya ulinzi aliopewa Dk. Dlamini-Zuma na aina ya vitisho alivyopokea.

Dk. Dlamini-Zuma anaonekana kuwa na nia ya kumrithi mumewe huyo wa zamani na ameshaanza kampeni.

Aidha amekuwa mstali wa mbele kumtetea Rais Zuma dhidi ya wakosoaji wanaomtaka ajiuzulu kutokana na mlolongo wa kashfa za ufisadi, upendeleo na ubadhilifu.

WAMAREKANI WAMTAKA TRUMP ATANGAZE KODI ALIYOLIPA SERIKALINI


MAKUMI kwa maelfu ya watu katika miji mbalimbali nchini hapa wameendesha wakitaka Rais Donald Trump atangaze kodi aliyolipa kwa Serikali, jambo ambalo yeye binafsi amekataa kulifanya.

Waandamanaji wengine walibeba sanamu kubwa za kuku, wakimaanisha Rais ni mwoga na amekataa kutoa takwimu za kodi yake.

Karibu watu 14 wametiwa mbaroni huko Berkeley katika jimbo la California ambako wafuasi wa Rais Trump na wapinzani wake walikabiliana.

Ingawa hakuna sheria inayomlazimisha Trump kutangaza kodi yake, marais wote wa Marekani wamekuwa wakifanya hivyo kwa muda wa miongo minne iliyopita.

Maandamano hayo yalipangwa kwenda sambamba na siku ya mwisho ya raia kuwasilisha takwimu zao za kodi.

VIJANA WATAKIWA KUJITAFUTIA FURSA


Na HARRIETH MANDARI,

VIJANA nchini wametakiwa kubadili mtazamo wa kuwa ajira ndiyo njia pekee ya kuwainua kiuchumi na badala yake wajikite kwenye sekta isiyo rasmi kwa kuanzisha biashara mbalimbali.

Naibu Waziri wa Kazi, Vijana na Ajira, Athony Mavunde, ameyasema hayo hivi karibuni, wakati akifungua mafunzo ya uhamasishaji wa ujasiriamali kwa vijana wa jijini Dar es Salaam.

Naibu Waziri huyo alisema, bado vijana wengi wana mtazamo kuwa ajira ndiyo njia pekee ya kuwa na maisha bora na ya uhakika.

Alisema takwimu za vijana walio kwenye sekta iliyo rasmi na isiyo rasmi nchini ya mwaka 2014, zinaonyesha vijana walio kwenye sekta rasmi ni kati ya 850,000 -1,000,000,000 na walio bado kwenye soko la ajira ni 150,000-200,000 na hivyo kuweka pengo la vijana zaidi ya 600,000 ambao hawana cha kufanya.

“Kama Serikali, tumekuwa tunachukua hatua kuondokana na changamoto hiyo ambapo imeanza kuwawezesha vijana mmoja mmoja na vikundi,” alisema Mavunde.

Alisema kuwa, tatizo linalokwamisha kundi hilo ni kukosa vigezo vya kukopesheka kwenye mabenki, hivyo kuwalazimu kukaa vijiweni bila kazi, japokuwa wengine tayari wana mawazo na mipango mizuri ya biashara.

“Lipo kundi la vijana ambao pamoja na kuwa hawakufanikiwa kusoma hadi ngazi za elimu ya juu, lakini wana vipaji vya ufundi, kilimo na vingine vingi, ambao pia serikali imeandaa mkakati wa kuwakwamua kiuchumi kupitia vipaji vyao,” aliongeza.

MCHUNGAJI RWAKATALE AMSHUKURU JPM


MCHUNGAJI Kiongozi wa Kanisa la Mlima wa Moto lililopo Mikocheni B, Assembles of God, Dk. Getrude Rwakatale, amemshukuru Rais Dk. John Magufuli kwa kumkumbuka na kumteua katika nafasi ya ubunge wa Viti Maalumu.

Dk, Rwakatale alitoa shukrani hizo Dar es Salaam jana wakati alipozungumza katika kanisa hilo wakati wa ibada ya Sikukuu ya Pasaka.

“Leo (jana) tunasherehekea kumbukumbu ya kufufuka kwa mwokozi wetu Yesu ambaye alitufia pale msalabani,… Pasaka ya mwaka huu ni yangu, Mungu ameniona.

“Nina furaha ya mwili na roho kwa sababu Yesu amefufuka na pia Mungu amenirudisha bungeni, Mungu amejibu maombi yetu, tulifunga siku tatu na ile ya mwisho akajibu,” alisema Mchungaji Rwakatale.

Alisema ana kila sababu ya kumshukuru Rais Dk. Magufuli kwa sababu wapo wanawake wengi ambao angeweza kuwachagua na kuwapa nafasi hiyo.

“Nakishukuru pia Chama Cha Mapinduzi (CCM) kwa kunikumbuka, wapo wanawake wangapi lakini leo mlima wa moto katikati ya maombi, Mungu ametenda,” alisema.

Dk. Rwakatale alitumia ibada hiyo kuwaomba msamaha watu aliowakosea huku akiwasihi waungane naye kumshukuru Mungu katika maombi.

“Katika Luka 24:1-9 tunasoma habari kuhusu ufufuko wa Yesu, tumezoea makaburini huwa kuna habari mbaya lakini kwa Yesu ilikuwa tofauti, ilikuja habari njema.

“Alitangaza msamaha hata alipokuwa msalabani basi naomba mnisamehe nilipokosea maana na mimi ni mwanadamu,” alisema.

Aprili 14, mwaka huu Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC), kupitia kwa Mkurugenzi wa tume hiyo, Ramadhan Kailima ilitangaza jina la Mchungaji Rwakatale kuwa mbunge baada ya Chama cha Mapinduzi (CCM) kupeleka jina lake.

Tume ilipitia fomu zake na kuridhika kuwa mteule huyo ana sifa za kuwa mbunge akichukua nafasi ya Sophia Simba ambaye alivuliwa uanachama na chama chake.

Machi 11, mwaka huu, Sophia Simba ambaye alikuwa Mwenyekiti wa Umoja wa Wanawake wa CCM (UWT) alivuliwa uanachama kwa madai ya ukiukwaji wa maadili ya chama hicho na hivyo kumfanya kukosa sifa ya kuendelea kuwa mbunge kwa mujibu wa Katiba ya Tanzania.

POLISI WANASA MTANDAO WA WEZI WA BAJAJI


Na ABDALLAH AMIRI,

JESHI la Polisi wilayani Igunga limenasa mtandao wa wezi wa bajaji ambao wamekuwa wakipora na kusababisha mauaji ya madereva wake kwa mwaka 2016 na mwaka 2017.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Tabora, Hamisi Selemani Issa alisema katika uchunguzi wa kina wamenaswa watu watutu ambao walikuwa wakijihusisha na matukio ya mauaji wa madereva wa bajaji na kuzipora.

Alisema tangu kuibuka matukio ya wizi wa bajaji mwaka jana, polisi walikuwa wakiendelea uchunguzi kwa miezi tisa na juzi waliwakamata watuhumiwa watatu ambao ni vinara wa matukio ya wizi huo na mauaji.

Aliwataja waliokamatwa kuwa ni Safari Anthoni (25), Safari Kija (22) ambao walikuwa madereva wa bajaji na John Emmanuel (30), wote wakiwa wakazi wa Wilaya ya Kahama mkoani Shinyanga.

“Tuliwakamata watu hawa baada ya uchunguzi wa miezi tisa, tumewakamata huko Kahama mkoani Shinyanga na katika uchunguzi tumebaini kuwa ndiyo waliojihusisha na mauaji ya waendesha bajaji watatu wa Kata ya Igunga mjini,” alisema.

Alisema baada ya kukamatwa watuhumiwa hao walifanya upekuzi majumbani kwao na kukuta wakiwa na bajaji tano, kati yake tatu ni za madereva wa bajaji waliouawa mwaka jana.

Bajaji tatu zilizotambuliwa ni zile zilizokuwa zikiendeshwa na Alex Okungu (30) aliyetekwa na kuuawa Agosti 16 mwaka jana, Songa Juma (24) aliyeuawa Desemba 10 mwaka jana na Maduhu Dwisha (35) aliyeuawa Machi 2 mwaka huu.

Polisi pia walikamata simu moja na kitambulisho, mali ya marehemu Maduhu Dwisha aliyeuawa Machi 2, mwaka huu na watuhumiwa walikiri kuhusika na matukio hayo.

Mkuu wa Wilaya ya Igunga, John Mwaipopo alipongeza polisi kwa kufanikisha kupatikana kwa bajaji zilizoibiwa pamoja na watuhumiwa.

Alisema matukio hayo yalikuwa yakisikitisha na kuwafanya wananchi kuilalamikia serikali.

Mwaipopo alisema kutokana na matukio hayo kushamiri, aliagiza bajaji zote mwisho wa kuendesha shughuli zake iwe saa 1:00 usiku.

Bank ya Exim yajipanga kutanua wigo wa utoaji huduma katika ukanda wa Afrika Mashariki


Ikiwa ni miaka 20 tangu kuanza kwake kutoa huduma kwa wananchi katika masuala ya kifedha, Benki ya Exim imejipanga kutanua wigo wake wa kibiashara wa utoaji huduma katika nchi mbalimbali za ukanda wa Afrika Mashariki.

Sambamba na Tanzania, tayari benki hiyo imeweza kupeleka huduma zake katika nchi za Comoro, Djibout na Uganda huku bado ikiendelea kufikiria kutanua wigo wake zaidi na zaidi. Mipango hiyo imeelezwa na George Shumbusho, Mkuu wa Hazina wa Exim Bank.

Shumbusho anasema “Miaka 20 ya mafanikio katika ukanda huu wa Afrika Mashariki, kwa maana ya Tanzania, Comoro na Djibout na Uganda, bado tunafikiri kuendelea kutanua mipaka yetu kutokana na mahitaji ya soko”.

Mbali na kutanua wigo wa utoaji huduma kwa wateja kulingana na uhitaji wa soko, Shumbusho anasema kuwa benki hiyo imeweka mkazo katika kutoa huduma bora zenye kuweka mbele maslahi ya mteja.

“Tunajikita zaidi katika kuhakikisha mteja ndio sehemu ya kati ya mtazamo wetu. Uwekezaji wetu unalenga katika kuhakikisha mahitaji ya kibenki ya mteja wetu yanapata suluhisho sahihi ndani ya Bank hii”, Anaongezea George Shumbusho.

Hii ina maana kuwa, licha ya Exim Bank kujipanga katika kuhakikisha inatanua wigo wa huduma kwa wateja wa ndani na nje ya nchi, lakini pia wanajipanga katika kutoa huduma bora kwa wateja wao hao ambao ndio kitovu kikuu cha biashara yao.

MAUAJI YA POLISI 8 SI UJAMBAZI WA KAWAIDA

Na WAANDISHI WETU

-KIBITI, DAR ES SALAAM

TUKIO la kuuawa kwa askari wanane waliokuwa wakitoka doria katika Kijiji cha Jaribu wilayani Kibiti, lina kila dalili kutekelezwa na watu wenye ujuzi na malengo mapana.

Tukio la sasa ambalo limechukua uhai wa Inspekta Peter Kigugu, F.3451 Koplo Francis, F.6990 PC Haruna, G.3247 PC Jackson, H.5503 PC Siwale, H.1872 PC Zacharia, H.7629 PC Maswi na H.7680 PC Ayoub, ni mwendelezo wa matukio mengine saba ya aina hiyo yaliyotokea katika kipindi kisichozidi mwaka mmoja Mkoa wa Pwani.

Ingawa hadi sasa si Jeshi la Polisi wala mamlaka nyingine ambazo zimekwishaeleza kwa uwazi kiini cha kuwako kwa mfululizo wa matukio ya aina hiyo katika maeneo yale yale, lakini utekelezaji wake na aina ya watu wanaotekeleza unaelezwa kuwa na mwelekeo wa kigaidi.

Timu ya MTANZANIA Jumamosi ilifika katika eneo la tukio na baadaye Kituo cha Polisi Bungu iliposhuhudia gari aina ya Toyota Land cruiser lenye namba za usajili PT 3713, lililoshambuliwa na wahalifu likiwa lina jumla ya matundu 22 ya risasi.

Upande wa kioo cha mbele cha gari hilo lilikuwa na matundu tisa, wakati ubavu wa kushoto ukiwa na matundu mawili na upande wa kulia juu kulikuwa na tundu kubwa moja na upande wa nyuma kukiwa na matundu sita.

Mmoja wa askari ambaye hakutaka jina lake kuandikwa gazetini, alisema wauaji hao walikuwa wamejificha kwenye magema yaliyopo pembezoni mwa barabara ya Kilwa.

“Ilikuwa ni vigumu kubaini sehemu ile kama kuna watu wanatuchora ndio maana ukiona hata haya matundu ya risasi yanaonyesha yalipigwa kutoka juu.

“Inatia hasira sana jinsi wenzetu walivyouawa, yule kiongozi wa patroo alikuwa kavaa kofia ngumu, tulikuta kapigwa risasi nane kichwani yaani tulivyomvua tu kofia ubongo wote ukamwagika,” alisema.

Aliongeza kwamba, wahalifu hao wanaonekana kujipanga siku nyingi kutekeleza mauaji hayo.

“Tulipokagua eneo walipotekeleza shambulio hilo nyuma ya gema kwa upande wa kulia kama unatoka Dar es Salaam tumekuta mazingira yanayoonyesha walikuwapo eneo hilo kwa siku zaidi ya tatu, kwenye ile mikorosho kulionekana kuwapo kambi na kunaonesha walikuwa wanapika pale pale,” alisema.

Askari mwingine ambaye naye hakutaja jina lake, alisema tatizo kubwa lipo katika jamii ambapo wananchi hawatoi ushirikiano wa kufichua mtandao wa wahalifu.

“Tumekuwa na operesheni ya muda mrefu ya kuwasaka wahalifu wanaotekeleza mashambulizi haya, kwa wale tunaowakamata kwa kuwahoji hata ukiwashurutisha vipi watakwambia neno moja astakafirulah!

“Wengine tukiwabana sana wanasema hawako tayari kusema chochote bora wauawe. Nakumbuka kuna wachache tu wametuambia kuwa wamepata mafunzo ya kufanya aina hiyo ya uhalifu katika mataifa 11 ya Afrika Kaskazini na Arabuni,” alisema askari huyo.

Askari mwingine alisema hajalala kwa siku ya nne jana kwa sababu alikuwa kwenye doria porini.

“Nilikuwa kwenye doria ..hawa wahalifu wanajificha sana huko porini wanajifanya wanachoma mkaa, tulikuwa tunabomoa nyumba kule, unakutana na mtoto wa miaka mitano jeuri kweli na ukimuuliza wazazi wake wako wapi anakujibu wamekufa kumbe wamejificha.

“Hivi juzi tulifikia nyumba moja huko kijijini kabla ya kuvamia kuwakamata tukasikia mzee anatoa maelekezo kwa mwanawe kwamba hao mapolisi ni makafiri tu ukikutana nao waue, uanze na wao kisha uhamie kwa walimu,” alisema askari huyo.

Timu ya MTANZANIA Jumamosi ilikutana na Waziri wa Mambo ya Ndani, Mwigulu Nchemba katika eneo la tukio ambaye ameelezea shambulio hilo kuwa ni la kuvizia na lilipangwa.

Mwigulu alitoa kauli hiyo jana baada ya kutembelea eneo ambalo shambulio hilo lilifanyika, akisema tukio hilo linachukiza hivyo Serikali haitashindwa vita hiyo.

Aliongeza kwamba tukio hilo limechochea zaidi nguvu ya kupambana na uhalifu wa aina yoyote hapa nchini.

“Nimekuja kuwapa pole askari wetu, tukio hili linaonekana lilipangwa na si bahati mbaya. Nawaomba Watanzania watulie sisi tumejipanga vizuri kupambana na uhalifu wa aina hii na tutazirudisha silaha zote ambazo wameziiba,” alisema Mwigulu.

Alisema kutokana na hatari ya eneo husika, ameagiza kuongezwa kwa askari pamoja na vifaa vya kutosha hususani magari makubwa.

“Sikutegemea kuona eneo lenye hatari kama hili kuwa na askari wachache pamoja na vifaa vichache,” alisema Mwigulu.

Wakati Mwigulu akisema hayo, kwa upande wake Kamishna wa Operesheni na Mafunzo, Nsato Mssanzya, akizungumza na waandishi wa habari Makao Makuu ya Jeshi la Polisi jijini Dar es Salaam jana, alisema alivitaka vyombo vya ulinzi na usalama kuungana kupambana na majambazi walioua askari hao.



Akielezea tukio hilo, Mssanzya alisema lilitokea katika Kijiji cha Jaribu Mpakani kilichopo Wilaya ya Kibiti Mkoa wa Pwani, ambapo askari tisa walikuwa wanatoka lindo na kurudi kambini.

Alisema askari hao wakiwa kwenye gari la wazi walivamiwa na majambazi ambao walimrushia risasi dereva hali iliyosababisha gari hilo kuyumba na kuanguka.

“Mara baada ya kutokea kwa tukio hilo, majambazi hao walivamia gari hilo na kuanza kuwapiga risasi askari waliokuwa ndani ya gari na askari wanane walifariki na mmoja alijeruhiwa mkononi,” alisema Mssanzya.

Aliongeza kuwa mara baada ya kuua polisi hao majambazi hao waliiba silaha saba, nne zikiwa SMG na tatu ni Long range ambazo zilikuwa zinatumiwa na polisi hao wakati walipokuwa lindo.

Alisema wakati majambazi hao wanakimbia, kulikuwa na askari wengine waliokuwa kwenye maeneo hayo ambao walianza mashambulizi na kufanikisha kuua majambazi wanne kati ya wale waliofanya tukio hilo na kuokoa silaha nne, mbili zikiwa za polisi waliouawa na mbili zinatumiwa na wao kwenye matukio mbalimbali.

Alisema matukio ya mauaji katika maeneo hayo yamekuwa yakitokea mara kwa mara jambo linaloonyesha wazi kuna vikundi vya majambazi vimejificha kwenye misitu iliyopo eneo hilo na hivyo kuhitaji nguvu ya ziada ili kuhakikisha wanavisambaratisha.

“Hatuwezi kuvumilia kuendelea kwa vitendo hivyo ambavyo vimekuwa vikijitokeza mara kwa mara katika maeneo hayo, sasa inatosha, dawa ya moto ni moto,” alisema Mssanzya.

Alisema hadi sasa zaidi ya polisi 10 wameuawa kwa vipindi tofauti katika maeneo hayo, mbali na baadhi ya watendaji wa Serikali ya kijiji.

“Imefika wakati sasa wa kuhakikisha wahusika wanakamatwa na kufikishwa kwenye mikono ya sheria.”

Aliwataka wananchi kutoa ushirikiano katika kipindi hiki cha msako wa watu hao ili wahusika waweze kukamatwa na kufikishwa kwenye mikono ya sheria.

Tukio hilo limemsikitisha na kumshtua Rais Dk. John Magufuli ambaye amesema analaani matukio yote ya kuwashambulia askari polisi ambao wanafanya kazi kubwa na muhimu ya kulinda raia na mali zao.

Rais Magufuli ametaka Watanzania wote watoe ushirikiano katika kukomesha vitendo hivyo.

“Nimeshtushwa na nimesikitishwa sana na vifo vya askari wetu wanane ambao wamepoteza maisha wakiwa wanalitumikia Taifa, naungana na familia za marehemu wote, Jeshi la Polisi na Watanzania wote katika kipindi hiki kigumu cha huzuni na majonzi ya kuondokewa na vijana wetu shupavu.

“Namwomba Mwenyezi Mungu atupe moyo wa subira, uvumilivu na ustahimilivu,” alisema Rais Dk. Magufuli kupitia taarifa iliyotumwa kwenye vyombo vya habari na Kurugenzi ya Mawasiliano Ikulu.

Kumekuwapo na mlolongo wa matukio ya mauaji katika wilaya ya Kibiti na Mkuranga na kinachozua maswali ni kitendo cha wauaji kutochukua mali yoyote.

Tukio la sasa la kuuawa kwa askari wanane limetokea ikiwa ni siku chache baada ya askari wa Jeshi la Polisi kuwaua kwa risasi wanaume watatu waliokuwa wamevalia buibui za kike.

Wanaume hao ambao walikuwa na pikipiki mbili, walikuwa wakijaribu kukwepa vihunzi vya polisi vilivyokuwa vimewekwa katika Daraja la Mkapa.



Februari mwaka huu, watu watatu akiwemo Ofisa Upelelezi wa Wilaya (OC CID) wa Wilaya ya Kibiti mkoani Pwani, Mrakibu wa Polisi, Peter Kubezya, waliuawa kwa risasi.

Wengine waliouawa ni Ofisa wa Misitu ambaye alikuwa Mkaguzi wa Kituo cha Ukusanyaji mapato ya ushuru katika Kijiji cha Jaribu, Peter Kitundu na Rashid Mgamba ambaye ni mlinzi/mgambo ambao walipigwa risasi kichwani na begani na walikufa papo hapo eneo la tukio.

Mei, 2016 Mwenyekiti wa Kijiji cha Nyambunda, Said Mbwana, aliuawa kwa risasi.

Oktoba, 2016 Ofisa Mtendaji wa kijiji hicho hicho, Aly Milandu, aliuawa kwa kupigwa risasi na watu wanne.

Novemba, 2016 wenyeviti wawili wa vitongoji wa kijiji hicho, waliuawa kwa kupigwa risasi.

Januari, 2017 watu ambao Jeshi la Polisi hadi sasa halijawafahamu walimuua mfanyabiashara, Oswald Mrope kwa kumpiga risasi mbele ya familia yake.

Februari 3, 2017 watu wasiojulikana walivamia nyumba ya mwenyekiti wa Kijiji cha Jaribu, Bakari Msanga na kuichoma moto huku yeye mwenyewe akifanikiwa kuwatoroka.

JPM: MTANIKUMBUKA


Na NORA DAMIAN-DAR ES SALAAM

RAIS Dk. John Magufuli amesema Watanzania watamkumbuka pamoja na awamu ya tano ya uongozi wake, ambayo imejielekeza kufanya kazi kwa bidii.

Kauli hiyo ya Dk. Magufuli imekuja mapema katika kipindi cha miaka miwili ya awamu ya kwanza ya utawala wake, tofauti na watangulizi wake, marais wastaafu Benjamin Mkapa na Jakaya Kikwete ambao waliitoa katika kipindi cha mwisho cha uongozi wao.

Februari 30, 2015, Rais wa Awamu ya Nne, Jakaya Kikwete, alitoa kauli inayofanana na ya Dk. Magufuli, wakati akizungumza katika Ofisi Ndogo za Makao Makuu ya CCM Lumumba, Dar es Salaam.

Kikwete alisema yeye anaondoka, lakini Dk. Magufuli ataendeleza kwa kasi kuanzia pale alipoishia.

“Naondoka mie tumeleta chuma hiki, pale nilipochoka mie yeye sasa anakwenda kwa kasi, anazo nguvu za kutosha kuliko mie.

“Na mlikuwa mnasema mie mpolepole, hivi sasa mabadiliko kuleta mkali… na ameanza kutema cheche,” alisema.

Jana wakati akizindua ujenzi wa reli mpya ya kisasa ya Standard Gauge (SGR), ambayo itatumiwa na treni ya umeme Pugu, Dar es Salaam, Dk. Magufuli alisema Watanzania wataikumbuka Awamu ya Tano ambayo ni ya kazi.

Alisema wakati wa kuomba kura, aliahidi mambo mengi ikiwamo kuimarisha miundombinu ikiwa ni pamoja na reli ya kisasa ambayo ilitakiwa ijengwe mwaka 1961.

“Uchumi unakua na ushahidi ni miundombinu tunayojenga, tumebana fedha za mafisadi, tumebana fedha za wapigadili, tumenunua ndege mpya sita, zitakuza utalii, biashara na kulifikisha lori letu linakotaka kwenda.

“Nawaambia siku moja mtaikumbuka awamu ya tano ya kazi, lakini nafahamu katika usafiri wowote unapopakia abiria uhitaji kuwauliza watasimama kuangalia sehemu gani wakati lori linaondoka.

“Wako watakaotazama nyuma, ubavuni, kule lori linakoelekea, kama ukipakia wasukuma wanaweza kuimba kwenye lori.

“Dereva mzuri hutakiwi kusikiliza nyimbo, kuangalia watu walikotazama, angalia unakolipeleka lori ili lifike salama. Kwa hiyo nawahakikishia mimi najiamini ni dereva mzuri na kwenye lori langu limepakia watu wa aina hiyo, wako wanaoimba, wanaopiga stori, wanaotazama nyuma wakati lori linakwenda mbele, walioangalia mbele, ubavuni, lakini lori litafika kule linakokwenda na hili ni lori la maendeleo.

“Na katika kazi tunazofanya, wanaopiga kelele ni wale waliozoea kupiga dili, waendelee, lakini lori litakwenda hadi linakotaka,” alisema Dk. Magufuli.

Alisema kuwa wapo watu wanacheza michezo michafu kwa lengo la kuvuruga amani nchini na aliwatahadharisha kwamba anajua anakokwenda, hivyo pasitokee mtu wa kubadilisha ajenda halafu waanze kuzungumzia ajenda ambazo haziko katika ilani ya uchaguzi.

“Katika nchi nyingi walizojaribu kupiga hatua, walichonganishwa na kugombana wenyewe kwa wenyewe, nawaomba tutangulize Tanzania kwanza siasa baadaye, Watanzania wanataka maendeleo, hakuna Mtanzania anayekula siasa… iacheni Serikali ya CCM itekeleze wajibu wake tutakutana 2020, sasa ni kazi tu,” alisema.



VITA YA UFISADI

Akizungumzia vita ya kupambana na ufisadi, Dk. Magufuli, alisema ni ngumu na ina mlolongo mwingi, hasa unapowabadilisha watu waliozoea maisha fulani kwa miaka 50.

“Samaki mkunje angali mbichi, akishakomaa mvunje tu. Na fisadi mkunje angali mbichi, akishakomaa mvunje na wakati wa kumvunja ni lazima atalalamika.

“Ni nafuu walalamike wachache, lakini wafaidike wengi. Ninapozungumzia mchanga, ningeweza kusema watangulize makontena yangu mawili Ulaya, lakini kutoka moyoni nafanya kazi kwa niaba yenu.

“Mlinituma nifanye, haya yote ninayofanya kweli ni mabaya? (wananchi wakaitikia mazuri).”

Akauliza tena: “Wangapi wanasema mazuri (wananchi wakanyoosha mikono), … kwahiyo niendelee? (wananchi wakaitikia)

“Tulionewa sana, tumechezewa sana, tumedharauliwa mno, Tanzania ni tajiri, hatutakiwi kuwa ombaomba. Tuna ubaya gani kwa Mungu, dhahabu zipo, wanyama wapo, lakini sisi ni masikini, ni lazima tujitambue,” alisema.

Kuhusu ujenzi wa reli hiyo, alisema yako mambo mengi aliyoahidi wakati alipokuwa akiomba kura kama kuimarisha miundombinu, ikiwamo ujenzi wa reli hiyo ya kisasa.

Alisema Watanzania wanapaswa kujivunia kujenga reli hiyo kwa fedha zao kwani sehemu kubwa ya reli ya kati ilijengwa na wakoloni (Wajerumani na Waingereza) kwa miaka 30 na reli ya Tazara iliyojengwa miaka ya 1970 ambayo ilijengwa kwa ufadhili wa China.



UJENZI WA RELI

Dk. Magufuli alisema awamu ya kwanza ya ujenzi wa reli hiyo itakuwa ni ya kilomita 300 ya kutoka Dar es Salaam – Morogoro na itagharimu Sh trilioni 2.7 na kwamba tayari mkandarasi amelipwa malipo ya awali wiki iliyopita Sh bilioni 300.

“Reli hii itarahisisha usafiri wa mizigo na abiria, itakuza biashara kati ya Tanzania na nchi nyingine, itakuza sekta zingine, itakuza utalii, itarahisisha usafirishaji wa malighafi na kutunza barabara. Barabara zetu nyingi zimekuwa zikiharibika ndani ya muda mfupi kutokana na kusafirisha mizigo mizito,” alisema Dk. Magufuli.

Kwa mujibu wa Dk. Magufuli, reli hiyo itaongeza fursa za ajira nchini ambapo watu 600,000 wanatarajiwa kuajiriwa zikiwamo ajira 30,000 za moja kwa moja.

Pia alisema Benki ya Dunia (WB) imetoa Sh bilioni 300 kukarabati reli ya zamani na Rais wa Uturuki amekubali kutoa mkopo wenye masharti nafuu kwa ujenzi wa awamu ya pili ya Morogoro hadi Dodoma.

Dk. Magufuli pia ameziagiza mamlaka husika kuhakikisha wananchi wa Pugu wanapewa kipaumbele katika fursa za ajira zitakazopatikana kwenye ujenzi huo.

Naye Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Profesa Makame Mbarawa, alisema reli hiyo itakuwa na uwezo wa kusafirisha tani milioni 17 za mizigo kwa mwaka, tofauti na reli iliyopo sasa ambayo ina uwezo wa kusafirisha tani milioni tano.

Alisema baada ya ujenzi kukamilika, mtu ataweza kusafiri kati ya Dar es Salaam na Morogoro kwa saa 1:15, Dar es Salaam na Dodoma saa 2:50 na Dar es Salaam na Mwanza saa 7:40.

“Tutamsimamia mkandarasi afanye kazi kwa uaminifu na kuhakikisha anajenga reli ya kisasa kwa viwango vya kimataifa,” alisema Profesa Mbarawa.



WAKANDARASI 40 WAOMBA KAZI

Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni Hodhi ya Rasilimali za Reli nchini (Rahco), Masanja Kadogosa, alisema wakandarasi 40 waliomba kazi ya kujenga reli hiyo na kwamba kampuni za Yapi Merkezi ya Uturuki na Mota-Engil ya Ureno ndizo zilikidhi vigezo.

Reli hiyo itakayokuwa na urefu wa kilomita 1,219 itajengwa kwa awamu tano na kwamba awamu ya kwanza ya kutoka Dar es Salaam hadi Morogoro yenye urefu wa kilomita 300 itagharimu Sh trilioni 2.7 na itajengwa kwa miezi 30.

Alisema kati ya kilomita hizo, 205 zitakuwa za njia kuu na 95 za reli ya michepuo ya treni kupishana na kupanga mabehewa.

Pia alisema kutakuwapo na vituo sita vya abiria na vituo vidogo sita vya kupishana treni.

“Reli hii itakuwa na urefu wa kilomita mbili, yenye mabehewa 100 yenye uwezo wa kusafirisha tani 10,000 kwa mara moja sawa na malori 500 yenye uzito wa tani 20 kila moja.

“Kutakuwa na mifumo ya mawasiliano ambapo dereva akiendesha kwa mwendo kasi atapewa onyo, akikaidi mwendo utapunguzwa kwa lazima ama treni itasimamishwa,” alisema Kadogosa.

Alisema zabuni za awamu nyingine nne za ujenzi wa reli hiyo zinatarajiwa kufunguliwa Aprili 19.

Awamu hizo ni za ujenzi kati ya Morogoro na Makutopora, Makutopora na Tabora, Tabora na Isaka na Isaka na Mwanza.

Kwa mujibu wa mkurugenzi huyo, awamu ya kwanza ya ujenzi pia itahusisha kutolewa mafunzo maalumu kwa Watanzania 300 kwa lengo la kuwapa ujuzi katika ujenzi, ukarabati na uendeshaji wa reli na treni zitakazotumika.

Naye Mwakilishi wa Kampuni ya Yapi Merkezi, Emre Aykar, alimuhakikishia Dk. Magufuli kuwa ujenzi huo utakamilika katika muda uliopangwa.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Bajeti, Hawa Ghasia, alisema bajeti ya miundombinu ya 2017/18 itapita bila matatizo na kwamba kwenye kamati ilishapita.

IBADA YA PASAKA: MAASKOFU WAONYA MAUAJI, UTEKAJI



IBADA YA PASAKA: MAASKOFU WAONYA MAUAJI, UTEKAJI
MATUKIO ya utekaji watu na kupotea kwenye mazingira yasiyoeleweka pamoja na mauaji ya polisi wanane mkoani Pwani, ni baadhi ya mambo yaliyotawala katika mahubiri ya mkesha na ibada za Sikukuu ya Pasaka katika maeneo mbalimbali nchini.

Maaskofu, wachungaji na mapadri wa makanisa mbalimbali katika ibada zao, walitumia muda mwingi kuzungumzia matukio hayo na kutahadharisha kuwa ni ishara mbaya ya kuporomoka kwa amani nchini.

Viongozi hao wa dini wanayatazama matukio hayo kwa sura mbili, kwamba yanafanywa na binadamu walio hai na binadamu wafu ingawa ni hai.

ASKOFU AMANI

Katika mahubiri yake, Askofu wa Kanisa Katoliki Jimbo la Moshi mkoani Kilimanjaro, Isack Amani, alisema vitendo vya utekaji nyara, biashara ya binadamu, mauaji ya askari, ubakaji na ulawiti na mengine yanayofanana na hayo, ni dalili ya amani na utulivu wa nchi kupotea.

Akihubiri katika ibada ya Pasaka iliyofanyika kitaifa katika Kanisa la Askofu la Kristo Mfalme, mkoani Kilimanjaro, Askofu Amani alisema vimekuwapo vitendo vingi vya uhalifu vinavyoendelea kutokea nchini yakiwamo mauaji ya ukatili ya askari, utekaji nyara na unyanyasaji wa raia, hali inayoonyesha kupotea kwa amani na utulivu nchini.

“Sasa majambazi wamefikia hatua ya kuua askari, hii ni ishara mbaya na wapo baadhi yetu wanashangilia. Inaonyesha kwamba ni makundi mabaya ya uhalifu tuliyo nayo kwenye jamii.

“Kwa lugha nyingine tunaweza kusema tunahitaji msaada kwa sababu hali si nzuri na inatishia amani, umoja na utulivu wetu.

“Amani na utulivu ni vitu ambavyo vinapaswa kuchochewa kama moto ila sasa naona mambo hayako sawa. Ni lazima wananchi pamoja na Serikali yetu tubadilike, tuichochee amani yetu,” alisema Askofu Amani.

Alisema pia kwamba kuendelea kufanyika biashara haramu ya binadamu ni jambo jingine linaloonekana kuchangia kuongezeka vitendo vya uhalifu.

“Biashara haramu ya biandamu huliingiza taifa lolote kwenye maafa mengi ya uhalifu kwa vile watu wamekuwa wanakodishwa na kufanya uhalifu. Hivyo basi, ni lazima Watanzania tubadilike na kuishi maisha yenye staha.

“Mauaji ya vikongwe na watu wenye ualbino, ushirikina, chuki, ubinafisi na kulipiza visasi ni baadhi ya mambo yanayoonekana kuidhoofisha nchi, hivyo ni lazima Serikali na wananchi wabadilike kulinda amani na utulivu.

“Wananchi tuungane na Serikali kulaani mambo yote ya uhalifu yanayoendelea nchini, tuliombee taifa letu ili wananchi tuwe na umoja katika kupambana na matendo ya uhalifu na uovu wote, na mkumbuke amani ya taifa letu ipo mikononi mwetu,”alisema.

Askofu huyo aliwataka wanasiasa wote nchini, waache ubinafsi kwa kufanya kazi za kuimarisha vyama vyao pekee na badala yake watumie muda huo kuwaletea wananchi wao maendeleo.

KATIBU MKUU TEC

Katibu Mkuu wa Baraza la Maaskofu wa Kanisa Katoliki Tanzania (TEC), Padri Raymond Sabba, alisema taifa linatakiwa kuombewa ili kuondokana na matatizo katika kipindi hiki cha mashaka ili mambo yanayojitokeza yasiendelee kutokea.

Akihubiri wakati wa mkesha wa Pasaka katika Kanisa Katoliki la Mtakatifu Joseph Dar es Salaam, Padri Sabba alisema kwa kiasi kikubwa yanayoendelea yanatakiwa kukemewa.

Alivitaja vitendo hivyo kuwa ni pamoja na mauaji ya kutisha, watu kutekwa nyara, ufisadi, uzembe wa viongozi, dawa za kulevya na kukosekana kwa haki.

"Tuliombee taifa katika kipindi hiki ambacho inawezekana kumekuwa na mashaka yakiwamo mauaji ya ajabu kwa watu wasio na hatia kama albino, vikongwe na kukosekana kwa haki.

“Kila mtu anapaswa kutambua kuwa hayo yote ni makaburi yanayopaswa kuondolewa kwa sababu hayampendezi Mungu kwa vile pia yanadhalilisha utu wa mtanzania.

“Wanaotenda matendo hayo wakati mwingine si wapagani bali ni wenye dini wanaojitambulisha kuwa ni wakristo wakati matendo yao hayafai,” alisema Padri Sabba.

Aliwataka wakristo kuhakikisha wanaliombea taifa katika kipindi hiki ambacho kuna mashaka juu ya mambo mbalimbali ya kutisha yanayoendelea nchini.

ASKOFU GAMANYWA

Askofu wa Kanisa la BCIC lililoko Mbezi Beach, Dar es Salaam, Sylvester Gamanywa, alisema matukio yanayotokea nchiniyana sura mbili.

“Hayo yanafanywa na binadamu walio hai na binadamu wafu ingawa ni hai. Kwa kifupi, yanafanyika mambo ya ajabu na ya kusikitikisha na ya kuudhi wakati mwingine.

“Huwezi kutoa uhai wa binadamu kama kitu cha mchezo. Tumeshuhudia mauaji ya polisi waliouawa Kibiti na si hao tu wameshauawa wengi. Tusishangae hayo ni matendo ya watu waliokufa kiroho.

“Kwa mateso aliyoyapata Yesu, tungeweza kuua askari wote kwa mkupuo, lakini Yesu badala ya kuua, alisamehe.

“Unapoona watu wanafanya vituko, mfano wazee wanafanya zinaa na watoto waliowazaa, hao ni wafu, wamekufa kiroho.

“Mara nyingi kifo cha roho huanzia kwenye kinywa cha mtu ambako maneno yake yanaweza kutoa majibu kama ni hai au mfu.

“Kama mtu anatoa maneno ya chuki, fitina, uchonganishi ama kupandisha watu hasira, hizo ni dalili za mauti ndani ya kinywa chake,” alisema Gamanywa.

Alisema pia kwamba licha ya kuwapo kwa mamlaka za dola nchini, bado mambo mengi yanayotendeka kwenye jamii yanadhihirisha mamlaka zimezidiwa kutokana na kuongezeka kwa maovu kuliko nguvu ya udhibiti iliyopo.

“Mfu wa roho yuko hai mwili, lakini utashi wa kufufuka ni hiyari yake mwenyewe. Majambazi, wazinzi, waongo na wachawi, wakiamua kusema Yesu fufua roho zetu tuwe viumbe wapya tutoke katika makaburi, wote wanaweza kufufuka na polisi wakakosa kazi,” alisema.

Askofu Gamanywa pia aliwashutumu baadhi ya viongozi wa dini kwa madai kuwa wamesahau wajibu wao na kufanya kazi ambazo hawajatumwa na Mungu.

“Sisi viongozi wa roho na hapa nawazungumzia wakristo, tunatarajiwa kuleta ufufuo wa roho za watu waliokufa, lakini tunafanya kazi nyingine ambazo hatujatumwa na Mungu.

“Matamko ya kukemea na kulaani ni staili ya wanasiasa, sisi tunayo mamlaka inatoka juu. Hivyo basi, maneno yetu yanatakiwa kuwa ni habari za ufufuo kwa wenye dhambi ambazo mamlaka za kawaida haziwezi kufanya bali Yesu pekee.

“Tukihubiri watu wakaacha maovu, watafanya kazi bila kusukumwa, wataacha kazi haramu na wataacha uvivu.

“Kama viongozi wa dini watashindwa kuwahubiria watu wakaacha kutenda maovu, basi kazi hiyo itakuwa imewashinda na itabidi wajiuzuru.

“Kama wewe ni mchungaji ama askofu halafu kuna watu wanaokufuata ibadani lakini bado ni waongo, wezi, wafitinishaji, ujue kazi imekushinda.

“Kabla hatujawaambia wanasiasa wajiuzuru, tunatakiwa tuanze sisi. Mimi natangaza sijiuzuru bali nitawaambia ukweli, kwamba Yesu Kristo amefufuka ni lazima umkubali na kumwamini ili ufufuke roho.

“We must speak the truth (lazima tuseme ukweli), hata kama kuna watu wana fedha nyingi na wanatoa sadaka kubwa ni lazima waambiwe ukweli,” alisema Askofu Gamanywa.

ASKOFU MKUU KKKT

Mkuu wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT), Askofu Dk. Fredrick Shoo, alisema matukio ya utekaji yanajenga hofu ya kutoaminiana ambayo si nzuri na ni hatari kwa nchi.

“Mambo haya yanahitaji uthibitishisho, hivyo ni vema uchunguzi ufanyike na ikithibitika hatua zichukuliwe kwa sababu yanazidi kuwatia hofu watu,” alisema.

IRINGA

Askofu wa Kanisa la Kiinjili la Kirutheri Tanzania (KKKT) Dayosisi ya Iringa, Blaston Gavile, alisema mauaji ya askari wanane yaliyotokea wiki iliyopita mkoani Pwani, yanasikitisha na watu wanatakiwa wafunge kwa ajili ya kuliombea taifa.

Akitoa salamu za Pasaka katika Usharika wa Kanisa Kuu mkoani hapa, Askofu Gavile alisema kazi ya wakristo si kulalamika bali ni kumgeukia Mungu na kumuomba aliepushe Taifa dhidi ya matukio ya utekaji, mauaji na mengine.

“Kazi ya wakristo si kulalamika mtaani kama ilivyo kwa mataifa mengine bali kazi yao kubwa ni kufunga na kuomba kwa ajili ya taifa.

“Tuendelee kuliombea taifa na Mkoa wa Iringa, tuseme Mungu yatosha kuendelea kusikia matukio ya ajabu ndani ya nchi yetu,” alisema Askofu Gavile.

Naye Askofu mstaafu wa Dayosisi hiyo, Dk. Owdenburg Mdegella, aliwataka Watanzania kuacha kupoteza muda kujadili mambo yasiyo ya msingi badala yake wajikite kujenga nchi.

SINGIDA

Askofu mstaafu wa Kanisa la Pentekoste (FPCT) mkoani Singida, Dk. Paulo Samweli, alitoa rai kwa madhehebu ya dini nchini, kuliombea taifa liweze kuondokana na umwagikaji wa damu kwa Watanzania wasio na hatia wakiwamo polisi.

Akihubiri katika ibada ya Pasaka katika Kanisa la Pentekoste mkoani humo, Dk. Paulo alisema mauaji ya polisi wanane Kibiti, Pwani hayavumiliki na kila mtanzania anapaswa kuyakemea yasijirudie.

Dk. Paulo alisema jukumu la polisi ni kulinda Watanzania wa madhehebu yote na wasiokuwa na dini na mali zao.

“Tukianza kuwaua kwa ukatili namna hii, nani atatulinda? Wewe ukimuua polisi ujue wazi kuwa unajiua wewe mwenyewe bila ya kujijua.

“Unyama huu haukubaliki mbele ya Mungu na kwa Watanzania wote, tuungane kuukomesha.

“Watu wasipofanya maombi vitendo hivyo vinaweza kusambaa sehemu mbalimbali nchini na matokeo yake nchi haitakalika tena.

“Shughuli za kumwabudu Mungu kwa uhuru mpana kama ilivyo hivi sasa zitakuwa ni ngumu na kujiletea maendeleo nako kutakuwa ni shida kutokana na kuwapo viasharia vya uvunjifu wa amani,” alisema Askofu Dk. Paulo.

RAIS MAGUFULI

Rais Dk. John Magufuli na mkewe Janeth Magufuli jana waliungana na waumini wa Kanisa la Africa Inland– Tanzania, Dayosisi ya Pwani, Pastorate ya Magomeni kusali Ibada ya Pasaka.

Pia walishiriki ibada hiyo katika Kanisa la Mtakatifu Petro lililopo Parokia ya Oysterbay, Dar es Salaam.

Katika ibada hizo, Askofu wa Kanisa la Africa Inland – Tanzania, Charles Salalah na Mkuu wa Jimbo Kuu Katoliki la Dar es Salaam, Mwadhama Polycarp Kardinali Pengo, waliongoza maombi ya kumwombea Rais Dk. Magufuli aendelee kutekeleza majukumu yake vizuri.

Askofu Salalah alimpongeza Rais Magufuli kwa kazi kubwa ya kurekebisha mambo yasiyofaa nchini ikiwamo kuwaondoa viongozi wanaotumia madaraka yao vibaya na kufuja mali za umma.

“Unafanya kazi kubwa ya kutumbua majipu, majipu unayoyatumbua wewe ni madogomadogo yaliyotokana na jipu kuu ambalo ni dhambi za mwanadamu.

“Na jipu hili lilitumbuliwa na Bwana Yesu. Kwa hiyo sisi Wakristo wenzako na waumini wengine, tunakuombea sana na tunakuunga mkono katika kazi hii nzito ya kutumbua majipu ya watumishi hewa, mishahara hewa, mikopo hewa na mengine mengi,” alisema Askofu Salalah.

Naye Kardinali Pengo alisema baraka zilizoletwa na Yesu Kristo aliyefufuka ni kwa ajili ya watu wote wakristo na wasio wakristo na alimtakia heri Rais Magufuli ili matumaini ya baraka hizo ziwafikie Watanzania wote.

Alimuombea Rais Magufuli kuwa imara katika changamoto na machungu anayokutana nayo katika uongozi wake.

Naye Rais Dk. Magufuli aliwashukuru wakristo wa Kanisa la Africa Inland na waumini wa madhehebu mengine ya dini kwa kuendelea kumwombea.

Aliwaomba waendelee kumwombea na pia waiombee nchi iendelee kuwa na amani, umoja, mshikamano na watu wachape kazi.

Habari hii imeandaliwa na Nora Damian na Asha Bani (Dar), Upendo Mosha (Moshi), Francis Godwin (Iringa) na Nathaniel Limu (Singida).

Mfumuko wa bei waongezeka


MFUMUKO wa bei wa Taifa kwa mwezi Machi, 2017, umeongezeka hadi kufikia asilimia 6.4 kutoka asilimia 5.5 mwezi Februari, 2017.

Kuongezeka kwa mfumuko huo kunamaanisha kuwa kasi ya upandaji wa bei za bidhaa na huduma kwa mwaka ulioishia Machi, 2017 umeongezeka ikilinganishwa na kasi ya upandaji ilivyokuwa kwa mwaka ulioishia Februari, 2017.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Ofisi ya Taifa ya Takwimu, gahirisi za bei zimeongezeka hadi 108.44 Machi 2017 kutoka 101.93 Machi 2016.

Taarifa hiyo inaonesha kwamba mfumuko wa bei wa bidhaa za vyakula na vinywaji baridi Machi, 2017 umeongezeka hadi asilimia 11.0 kutoka asilimia 8.7 ilivyokuwa Februari, 2017.

Mfumuko wa bei kwa kipimo cha mwaka kwa bidhaa za vyakula nyumbani na migahawani kwa Machi, 2017 umeongezeka hadi asilimia 11.7 kutoka asilimia 9.3 Februari, 2017 huku badiliko la fahirisi za bei kwa bidhaa zisizo za vyakula likiwa limebaki kuwa asilimia 3.6 Machi, 2017 kama ilivyokuwa Februari, 2017.

Aidha, mfumuko wa bei ambao haujumuishi vyakula na nishati kwa Machi, 2017 umebaki kuwa asilimi 2.2 kama ilivyokuwa Februari 2017.

Taarifa hiyo ilisema fahirisi inayotumika kukokotoa aina hiyo ya mfumuko wa bei, haijumuishi vyakula vinavyoliwa nyumbani na migahawani, vinywaji baridi, petroli, dizeli, gesi ya kupikia, mafuta ya taa, mkaa, kuni na umeme.

Muhongo ahimiza elimu kukuza uchumi


MBUNGE wa Jimbo la Musoma Vijijini na Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo amewaomba wananchi kuweka nia kubwa katika sekta ya elimu ili kukuza uchumi wa familia na Taifa.

Akizungumza katika vijiji vya Bugoji, Muhoji, Chumwi Mgango na Bwai katika ziara yake ya kukagua ujenzi wa vyumba vya madarasa alisema bila kuwapatia elimu bora watoto, hali ya baadaye ya familia nyingi na hata taifa itakuwa shakani.

‘’Elimu ndio suala la msingi katika kupatia msingi bora wa elimu mtoto ili hapo baadaye aweze kulinufaisha Taifa. Katika masuala yote toeni kipaumbele katika elimu, afya na kilimo ambavyo ndio vya msingi na hapo,” alisema Muhongo.

Aidha, amewataka wananchi kuacha kulalamika na badala yake waongeze bidii katika utendaji wa shughuli za maendeleo, ikiwemo kilimo ili kuweza kuondokana na matatizo mbalimbali ya maisha.

Akizungumzia juu ya mradi wa maji aliwataka madiwani kusimamia suala la maji kwa kuhakikisha kwamba wanaliwekea kipaumbele kwenye vikao vyao ili kumuwia rahisi yeye kulibeba.

“…ndugu zangu mkitaka miradi iwe na uwezo na isiyo na uwezo ni lazima maombi yenu yawe rasmi na kuwa rasmi ni lazima madiwani wayajadili kwenye vikao vyao katika halmashauri,’’ alisema.

Kuhusu upungufu wa chakula, alisema wakati umefika kwa wananchi kuacha kutegemea mvua katika kilimo na kuanza cha umwagiliaji.

Naye Katibu wa Mbunge wa jimbo hilo, Ramadhan Juma alisema Profesa Muhongo amekwishaleta vifaa vya ujenzi ambapo jumla ya mifuko ya saruji ipatayo 1,269 na mabati 5,120 kwa ajili ya ujenzi wa madarasa katika shule za msingi 111 na sekondari 20 ambapo mgawanyo wa saruji katika ukanda wa Bukwaya shule 13, kati shule 18, ukanda wa Mugango 13 kati ya 24, ukanda Majita 40 kati ya shule 69.

Vita Vikuu vya Dunia vinakaribia? Juma la wasiwasi kuhusu Marekani na Korea Kaskazini


Ukafuatilia matukio, mijadala na ujumbe katika mitandao ya kijamii, unaweza kudhani Vita Vikuu vya Tatu vya Dunia vinakaribia.

Rais wa Marekani Donald Trump na Kiongozi wa Korea Kaskazini Kim Jong-un wamekuwa wakijibizana vikali kuhusu mpango wa Korea Kaskazini kuendelea kustawisha silaha za nyuklia na pia kufanyia majaribio makombora, jambo ambalo taifa hilo haliruhusiwi na Umoja wa Mataifa.

Marekani ilituma kundi la meli zake za kivita karibu na Korea Kaskazini, jambo ambalo liliikera Korea Kaskazini.

Trump aionya tena Korea Kaskazini

Uhusiano kati ya nchi hizo mbili haujakuwa mzuri tangu kumalizika kwa Vita Vikuu vya Pili vya Dunia.

Hata hivyo wiki iliyopita uhasama ulizidi na kufikia kiwango cha juu kuliko awali.

Jumatatu - Meli za kivita za Marekani

Rais Trump aliagiza kundi la meli za kivita za Marekani pamoja na meli moja yenye uwezo wa kubeba ndege na pia kutumiwa na ndege hizo kupaa na kutua, zielekee upande wa Korea Kaskazini.

Trump apuuzilia mbali mpango wa Korea Kaskazini

Taifa hilo limetekeleza majaribio kadha ya silaha za nyuklia na hilo halijaifurahisha Marekani.

Rais Trump alisema Marekani imejiandaa kuchukua hatua kivyake, bila usaidizi wa China, kukabiliana na tishio la nyuklia kutoka kwa Korea Kaskazini.

Jumanne - Kim amjibu Trump

Kim Jong-Un hakufurahishwa na hayo na alimjibu vikali Bw Trump.

Korea Kaskazini yamtaja Trump kwa mara ya kwanza

Trump apuuzilia mbali mpango wa Korea Kaskazini

Wizara yake ya mambo ya nje ilinukuliwa ikisema hatua hiyo ya Marekani ni ya "kipumbavu" na ikaahidi kujilinda "kwa nguvu zote za kivita."

China, ambao ni mshirika wa karibu zaidi wa Korea Kaskazini, walionya kwamba wataingilia kati na kutoa adhabu kali zaidi za kifedha kwa Korea Kaskazini iwapo taifa hilo lingefanya majaribio zaidi ya makombora.

Jumatano - China yazungumza

Vyombo vya habari vya China vilisema rais wa taifa hilo alimpigia Rais Trump kutuliza hali.

Marekani huenda isizuie makombora ya Korea

Rais Trump mwenyewe aliandika kwenye Twitter kwamba alikuwa amewasiliana na Rais Xi Jinping.

Bw Xi alidaiwa kumwambia Trump kwamba anataka amani na utahibiti eneo hilo na kwamba anaunga mkono pia juhudi za kumaliza silaha za nyuklia katika rasi ya Korea.

Alhamisi- Gwaride la wanajeshi

Korea Kaskazini ilizindua mpango wake mpya wa ujenzi wa nyumba za makazi na biashara mjini Pyongyang.

Ulionekana kuwa mpango wa kawaida tu, lakini ilikuwa pia fursa ya taifa hilo kuonyesha nguvu zake.

Waandishi wa habari wa mashirika ya kigeni walialikwa kushuhudia wanajeshi wakifanya gwaride na kutembea kwenye barabara za mji huo.

Donald Trump hakufurahishwa na hilo.

Aliandika tena kwente Twitter kwamba Marekani iko tayari kukabiliana na Korea Kaskazini.

Ijumaa- Onyo la China

China ilitahadharisha kwamba mzozo mkubwa kati ya Marekani na Korea Kaskazini "unaweza kutokea wakati wowote".

Ilizionya nchi zote mbili kukoma kurushiana vitisho, na kusema hakuwezi kuwa na mshindi katika vita.

Hayo yakijiri, Korea Kaskazini ilikuwa inakamilisha maandalizi ya gwaride kubwa na maonyesho ya kijeshi Jumamosi.

Jumamosi - Vifaru barabarani

Korea Kaskazini iliadhimisha miaka 105 tangu kuzaliwa kwa mwanzilishi wa taifa hilo Kim Il-sung.

Vifaru zilitolewa barabara za Pyongyang. Serikali ya Korea Kaskazini pia ilionyesha hadharani kwa mara ya kwanza makombora yanayoweza kuruka kutoka bara moja hadi jingine, na pia makombora ya masafa marefu yanayoweza kurushwa kutoka kwenye nyambizi.

Maafisa wa serikali ya Korea Kaskazini waliionya Marekani dhidi ya kuchukua hatua zozote, wakisema nchi hiyo iko tayari kwa vita.

Walisema watajibu kwa "mashambulio ya nyuklia".

Marekani: Hatutaivumilia tena Korea Kaskazini

Hayo yakijiri, Makamu wa Rais Mike Pence alielekea Korea Kusini kujadiliana na washirika wa Marekani kuhusu njia bora zaidi za kukabiliana na Korea Kaskazini.

Jumapili - Jaribio la makombora

Marekani ilidai kwamba Korea Kaskazini ilijaribu kurusha kombora, lakini likalipuka sekunde chache baada ya kupaa angani.

Inasadikika kwamba lilikuwa kombora la masafa marefu, ambalo hupaa juu anagani kwanza na ambalo huelekezwa, lakini baadaye huanguka hadi pahali ambapo panalengwa kutokana na mvuto wa dunia.

Umoja wa Mataifa umeipiga marufuku Korea Kaskazini kufanya majaribio kama hayo.

Rais Trump atachukua hatua gani?

Ni yeye mwenyewe pekee ajuaye jibu - au labda mwenyewe binafsi amekanganyikiwa!

Fate of the Furious yavunja rekodi ya dunia


Filamu ya Fate of the Furious imevunja rekodi ya dunia ya kuwa filamu iliyouzwa sana baada ya kuzinduliwa rasmi.
Filamu hiyo, ambayo ni ya nane katika mwendelezo wa filamu za Fast & Furious, ilipata mauzo ya jumla ya $532.5m (£424.7m) duniani wikendi ya Pasaka.

Hayo ndiyo mauzo ya juu zaidi duniani kwa filamu yoyote siku zake za kwanza baada ya kuzinduliwa rasmi.

Filamu hiyo imepita mauzo ya $529m (£421.8m) rekodi ya awali iliyowekwa na Star Wars: The Force Awakens.

Jina la filamu ijayo ya Star Wars latangazwa

Mauzo hayo ya filamu hiyo nchini Marekani hata hivyo yalikuwa chini ukilinganisha na mauzo ya filamu iliyotangulia.

Furious 7 ilipata mauzo ya $147.2m (£117.3m) nchini Marekani ilipozinduliwa 2015.

Lakini filamu ya sasa imezoa $100.2m (£80m) pekee.


Licha ya kushuka kwa mauzo yake Marekani, filamu hiyo bado ilichangia sehemu kubwa ya mauzo ya filamu Marekani, ambapo ilichangia karibu theluthi mbili.

Mshindani wake wa karibu alikuwa The Boss Baby, ambayo iliuza $15.5m na kuwa ya pili.

Filamu za Fast & Furious zilianza kuuzwa 2001.

Ufanisi wa filamu hii ya sasa ulichangiwa sana na China ambapo mauzo yake yalikuwa $190m (£151m) kwa siku hizo tatu.

Vin Diesel, ambaye ameigiza katika kila filamu ya Fast & Furious amesema anashukuru sana na amefurahishwa sana na ufanisi wa filamu hiyo.

Wengine walioigiza katika Fate of the Furious ni Charlize Theron, Tyrese Gibson na Ludacris.

Filamu nyingine za Furious zitatolewa mwaka 2019 na 2021.

Ombi la kutaka kuhalalisha bangi Kenya laungwa mkono


Zaidi ya Wakenya 1,400 wanaunga mkono ombi la kutaka kuidhinishwa kwa matumizi ya mmea wa bangi baada anayewasilisha hoja hiyo kuwawasilisha ombi lake mbele ya bunge la seneti.
Iwapo ombi hilo la mtafiti Gwada Ogot litaidhinishwa haitakuwa haramu kupanda ama hata kuuza bangi nchini Kenya.

Gwada Ogot anasema kwamba matumizi ya kiafya pamoja na utumizi wa mmea huo viwandani unaojulikana kwa jina la sayansi kama Cannabis sativa una faida nyingi.

Anasema kuwa matumizi ya mmea huo yataimarisha hali ya uchumi.

Sheria ya Kenya inapiga marufuku utumizi wowote wa bangi na kwamba mtu yeyote atakayepatikana akitumia dawa hiyo atashtakiwa kwa uhalifu.

Ogot anaomba bangi kuondolewa miongoni mwa orodha ya vitu haramu na kutaka sheria mpya kuanzishwa ili kuweka bodi simamizi ya utumizi wa mmea huo.

Ogot pia anataka watu wanaohudumia vifungo kwa kumiliki ,kupanda ,kusafirisha kuuza ama kutumia bangi kuachiliwa huru.

Mtafiti huyo ambaye amekiri kuvuta bangi wakati alipokuwa kijana amesema kuwa mataifa mengi katika bara Ulaya na Asia pamoja na majimbo kadhaa nchini Marekani yamehalalisha utumizi wa Marijuana.

Aliorodhesha Colombia, Mexico, Jamhuri ya Czech, Costa Rica,Ireland ,australia, Jamaica na Ujerumani kama mataifa yaliohalalisha utumizi wa mmea huo.

Mourinho: Manchester United waliwadhibiti Chelsea


Meneja wa Manchester United Jose Mourinho amesema vijana wake walifanikiwa "kuwadhibiti" viongozi wa ligi ya England Chelsea na kuwalaza 2-0 Jumapili uwanjani Old Trafford.
Mourinho alikuwa ameumizwa na Chelsea msimu huu mechi za awali tangu ahamie United.

Alikuwa amelazwa 4-0 ligini mechi ya kwanza msimu huu ugenini Stamford Bridge na pia alishindwa robofainali katika Kombe la FA pia uwanjani Stamford Bridge.

Msimamo wa ligi ya EPL 2016/17
'Yuda' Mourinho 'bado anaongoza Chelsea'

Lakini Mreno huyo hakuzidiwa wakati huu ambapo aliwapanga pamoja Marcus Rashford na Jesse Lingard safu ya mshambulizi na akampumzisha Zlatan Ibrahimovic.

Rashford alitangulia kufunga na Ander Herrera, ambaye alimdhibiti vilivyo Eden Hazard ,alifunga la pili kipindi cha pili.


Baada ya mechi, Mourinho alisema "Ni mpango ule ule wa wachezaji 11 ambao ulifanya kazi katika Kombe la FA uwanjani Stamford Bridge. Ndio bora zaidi kwa kucheza kaunta kote nchini na tuliwadhibiti vilivyo.

"Nimefurahishwa sana na vijana wangu. Nina furaha isiyo na kifani - na si kwa sababu ni Chelsea, ni kwa sababu tulihitaji alama hizo tatu.

"Sihisi furaha zaidi kwa sababu ya kulaza Chelsea - tuliwalaza viongozi wa ligi. Haijalishi kama kiongozi wa ligi ni Chelsea au klabu nyingine - tuliwachapa vizuri. Hakuna anaweza kusema hatukufaa kushinda mechi hiyo."

United watakuwa wenyeji wa Anderlecht mechi ya marudiano Europa League Alhamisi, mambo kwa sasa yakiwa 1-1 kutoka kwa mechi ya kwanza.

Watarejea ligini kucheza dhidi ya Burnley Jumapili.

Chelsea nao watakutana na Tottenham nusufainali Kombe la FA Jumamosi ijayo.

Mechi yao ijayo ligini itakuwa nyumbani dhidi ya Southampton.

Timu ya AC Milan yanunuliwa na kampuni ya China

Timu ya kandanda ya AC Milan ya Italia imeuziwa kampuni moja ya Uchina na kutia kikomo umiliki wake na aliyekuwa wakati mmoja Waziri Mkuu wa nchi hiyo na tajiri Silvio Berlusconi.
Kampuni ya China Rossoneri Sport Investment Lux, imekamilisha mkataba wa kuinunua timu hiyo kwa kima cha dola milioni 628, huku ikiwa na matumaini ya "kuongeza faida mara dufu".

Klabu hiyo ya Serie A imekuwa chini ya umiliki wa bilionea Silvio Berlusconi, tangu mwaka 1986.

Katika kipindi hicho chote, AC Milan ilifaulu kunyakua mataji manane katika ligi kuu na kunyakuwa kombe la vilabu bingwa barani Ulaya mara tano.

Aidha, Milan haijawahi kushinda mechi za Seria A tangu mwaka 2011 na imemaliza katika nafasi ya 7, 10 na 8 katika misimu mitatu iliyopita.

Kwa sasa inashikilia nafasi ya 6 katika ligi kuu, alama 20 nyuma ya vinara Juventus.

Mkenya Sarah Ikumu Ashangaza Kwa kipaji Britain's Got Talent Uingereza


Kijana Mwingereza ambaye wazazi wake Wakenya amevuma sana mtandaoni baada ya kusisimua kwa wimbo katika shindano la vipaji katika sanaa Uingereza la Britain's Got Talent Jumamosi.

Sarah Ikumu, 16, aliyezaliwa Uingereza, aliwashangaza wengi katika kipindi cha vipaji cha Britain's Got Talent, alipoimba wimbo wa And I'm Telling You ambao unadaiwa kuwa mgumu sana kuuimbwa ipasavyo.

Wimbo huo wake Jennifer Holliday ulitumiwa kwenye filamu ya Dreamgirls iliyotolewa mwaka 2006.

Uimbaji wa Sarah uliwaacha waliohudhuria mashindano hayo wakiwa wameduwaa huku wote wakisimama na kumshangilia.

Kilele cha uimbaji wake kikifika pale mmoja wa majaji ambaye anajulikana kuwa mgumu kufurahisha, Simon Cowell, alipobonyeza kengele ya dhahabu ambayo humpeleka mshiriki moja kwa moja hadi nusu fainali ya mashindano hayo.

Daktari Mtanzania atambuliwa Marekani

Sarah ambaye anasomea Milton Keynes alianza kuimba akiwa na miaka mitano huku akishiriki kwa mashindano kadha ya nyimbo.

Lakini hili ndilo shindano la kwanza ambalo anasema kuwa ni ndoto ambayo imetimia, mwanzo pale Jaji Simon alipompongeza kwa talanta yake akimuambia "lilikuwa jambo la kushangaza kwa mtu rika lake kusimama mbele ya watu akiwa na hofu na kuelekea kuimba wimbo ni kama ameutunga mwenyewe".

Mwimbaji mashuhuri ambaye pia ni jaji Alesha Dixon alimwambia Sara kuwa "'hakubaliwi' kuwa na talanta kama hii katika umri wake"

Majaji wengine wawili wakiwemo David Williams, Amanda Holden pia walimmiminia pongezi.

Mitandao ya kijamii ilifurika watu wakimsifu.

Trump Awapigia Simu Marais Wa Korea Kusini Na Japan


Rais mteule nchini Marekani Donald Trump ameihakikishia Korea Kusini kuwa, atadumisha uhusiano mzuri uliopo kati ya Marekani na Korea Kusini, kwa mujibu wa rais wa Korea Kusini Park Geun-hye.

Trump aliahidi wakati ya mawasiliano ya dakika kumi kwa njia ya simu siku ya Jumatano kuwa, nchi hizo zitadumisha ushirikiano uliopo na kujilinda kutokana a na kile alichokitaja kuwa msukosuko uliopo Korea Kaskazini.

Ofisi ya Park ilimnukuu Trump akisema, "tutakuwa nanyi kwa asilimia 100."

Mwezi Machi wakati wa mahojiano na gazei la New York Times, Trump aliilaumu Korea Kusini kwa kukosa kulipia maelfu ya wanajeshi wa Marekani walio nchini humo, na kutishia kuwa anaweza kuwaondoa ikiwa atachaguliwa.

Matamshi yake yalikaribishwa na Korea Kusini wakati huo..

Trump pia alizungumza na waziri mkuu wa Japan Shinzo Abe, kulingana na maafisa nchini Japan. Msemaji wake alisema kuwa Abe na Trump walizungumzia umuhimu wa ushirikiano kati ya Japan na Marekani ambapo walipanga kukutana baadaye mwezi huu.

Park Geun-hye: Aliyekuwa Rais wa Korea Kusini ashtakiwa kuhusu rushwa



Rais wa South Korea aliyeondolewa mamlakani Park Geun-hye ameshtakiwa rasmi kuhusiana na kashfa ya rushwa iliyopelekea kung'atuliwa kwake uongozini.

Viongozi wa mashtaka wanasema kuwa mashtaka yanayomkabili ni kupokea hongo, utumizi mbaya wa mamlaka, na kudukua siri za serikali.

Park, 65, ambaye yupo kizuizini, ameshtakiwa kwa kumruhusu rafiki yake wa karibu Choi Soon-sil kutoza fedha kampuni kadha kuu ili wapendelewe kisiasa.

Wanawake wote wawili walikana mashtaka.

Bi Park alitolewa ofisini mwezi uliopita.

Alipoteza kinga yake na kutolewa mamlakani baada ya mahakama ya kikatiba kuidhinisha uamuzi ya bunge kumng'atua uongozini.

Mkuu wa Samsung akamatwa Korea Kusini
Rais wa zamani Korea Kusini akamatwa
Rais wa Korea Kusini alihusika kwenye ufisadi

Bi Choi anatuhumiwa kutumia uhusiano wake wa kirais ili kuweka shinikizo kwa kampuni kutoa mamilioni ya madola katika michango kwa mashirika yasiyo ya serikali ambayo anayashikilia.

Bi Park anadaiwa kuhusika binafsi katika masuala hayo, na kumpa Bi Choi ruhusa isiyokubalika kupata nyaraka rasmi.

Kati ya kampuni hizo, ni kampuni kubwa nchini humo, Samsung.

Kaimu Kiongozi wake Lee Jae-yong na Bi Choi wamewekwa pamoja kizuizini huku Bi park akingojea kesi dhidi yake ianze.

Mwenyekiti wa kampuni ya Lotte Shin Dong-bin alishtakiwa kutoa rushwa Jumatatu, lakini viongozi wa mashtaka hawakumweka kizuizini.

Wote wawili, Samsung na Lotte wamekanusha mashtaka dhidi yao.

Hwang Kyo-ahn, ambaye ni mwaminifu kwake Bi Park, ndiye kaimu rais huku uchaguzi ukitarajiwa kufanyika tarehe 9 mwezi Mei.

Why, There Are No New Social Networks


There’s the big five — Facebook, Twitter, Instagram, Pinterest, and Snapchat — and then a series of fringe social media services unable to break through with invention. Why are we stuck in a cycle of sameness?

Your iPhone used to be a digital laboratory — a place for experiments in the form of apps. Try this, sure. Download that, why not? Somewhere along the line, that interest in dabbling wore off. Being convinced to try a new app became a monumental feat, and the folder hit hardest by this — the one that now holds the same four to five apps and never grows — was social.

There can be new apps, sure — if someone tells me there’s a new Google Drive–related app, I’m in. Or something (anything) for improved photo storage, yes. But joining another social network is a request I cannot entertain. The excitement over the new social media network Mastodon is fun — I’ve enjoyed reading about the open source Twitter alternative, but then I think … remember how much we all loved Peach?

According to a 2017 Pew report, more and more adults are using social networks, and though user growth is comparatively slowing for major social networks, it’s still growing. The report listed the five most popular social networks as Facebook, Instagram, Pinterest, Twitter, and … LinkedIn. These are the same platforms it listed in 2016. (The fact that Snapchat is missing should come as no surprise, given this is a survey of, ahem, adults.) And Pew found that these numbers grew for the networks between 2012 and 2014.

“I think what you’re seeing is that general purpose social networks are dominated by Facebook, Twitter, LinkedIn, and others, and that cracking into these market share leaders is a tall order for anyone,” Gartner analyst Brian Blau told me via email. “There is also a trend that smartphone users are not downloading as many apps today as they did in the early days of mobile technology. That means any new app has a significant challenge to get exposure, users, and loyalty.”

The inclination to download every new social app has dwindled significantly — things like storage space, signing up for yet another network, and terrible App Store discoverability are reason enough to forgo the latest attempt at Snapchat-esque ubiquity.

The latest attempt is Wuu, a Snapchat-like app I first saw advertised on Instagram. (Know your audience, I guess.) Wuu was created by Paul Budnitz, the same mind behind Ello. It’s still around, but pivoted into a “creators network” instead of an alternative to major social platforms. Within days of Wuu grabbing a few headlines, we were also talking about Mastodon. Oh yeah, and we met Apple’s video app, Clips. Before that there was the hype over Gab. (Ugh.) And again, Peach. Remember Vine? (RIP.)

I don’t begrudge anyone the excitement of a new social app. It’s easy to get caught up in the idea that something, anything different and unexpected could upend what’s become an increasingly homogenous landscape. And there was a period of time when disruptors had a shot at changing what the world of social platforms looked like — a few of them managed to do it, in fact. Hipstamatic and Instagram (admittedly, more one than the other) managed to push us into singular, image-based feeds, eschewing status updates and chat boxes for retro-ified photos. Before that, Twitter introduced real-time communication and news. (And eggs, and trolls, and a new destination for digital hate crime, etc.) Snapchat, of course, completely destroyed social media sameness with ephemeral messaging and disappearing photos, not to mention a mobile-only user interface that looked nothing like the design to which we’ve become acclimated.

At some point, though, the “Is it an app or a feature?” question became more pressing. Attempts to evolve platforms, like Google+, offered too much of the same (just slightly different, or in many cases, slightly nicer). Others, like Vine or Peach, added new, fun features that mainstays like Facebook and Twitter didn’t have — but those features were easy to appropriate into their own systems. (Boomerang from Instagram, for example, lacks the casualness of Vine, but certainly took a stab at its functionality.)

Going niche is a risk for any social media platform — but it feels like the only option most developers have now. Then again, take the emoji-only social network the tech media spent a day proselytizing. It turned out to be a joke and never actually launched. The List app — wherein you could compose and publish lists — befell a similar fate: Propped up by its famous founder, B.J. Novak, it captured our attention for a handful of weeks — it was not a joke, and it’s still around, but it’s certainly not disrupting how we use social media. Beme (propped up by a less famous founder, Casey Neistat) was a confusing if compelling idea that slid down the App Store charts before shuttering last November. And yet the cautious excitement around these products captures our desperation for something else.

In their wake is a sea of sameness. Facebook bought Instagram, both of which are swiftly morphing into Snapchat, easily the most inventive (if confusing) thing that’s happening to social media. Twitter and Facebook trade features, morphing into one another less conspicuously but doing exactly that nonetheless. Outliers like Tumblr and (to a lesser degree) Yik Yak can hold their own, but haven’t managed to reinvent how we communicate en masse. The emergence of something new feels almost impossible, and worse yet, it feels like the methods these social networks use may become identical. But it’s not all bleak.

“Social apps are now focused on messaging, and certainly it’s a vibrant area of innovation and advancement,” Blau told me. “So I wouldn’t say that all social apps are stagnating.” Maybe the copycat cycle will just push us away from public-facing social apps altogether and into private messaging, an arguably more inventive (and in some cases, nicer) space. It seems that the only time someone is able to create a new social network, it’s by accident. Venmo is not a social app — at least, it wasn’t intended to be. The PayPal-owned payment system was launched as a dead simple way to share money, complete with a few lighthearted features like emoji and a real-time feed of users’ transactions. This feed ultimately became a sort of social network within the app: It fuels FOMO, forces us to consider the financial side of dating, and even acts as a window into modern drug culture.

Venmo didn’t set out to be a better Twitter or a Facebook alternative; it took a fact of daily life that wasn’t all that interesting and certainly not very “social,” and created new digital communication behaviors. It was accidentally inventive.

“It’s harder for apps to break into the mainstream now, especially when it comes to social,” comScore’s Adam Lella told me via email — but he also pointed me to research the company had done about social app behavior. True, older users — 35 and older — were narrower in their social media use to the tried and true networks. Younger users, though, were still downloading new apps, and Snapchat’s ability to rise through the ranks and break into the top of the App Store was largely fueled by this. That willingness to try new apps, however, doesn’t always translate to sticking with them.

It’s also worth noting that just last year, comScore also compiled an infographic Lella shared with me asking if we’ve reached “peak app,” which found that people are downloading fewer apps than ever, and that our smartphone time is being spent using our favorite ones. And those are exactly what you think they are — the big names.

Product Hunt’s social editor and writer, Niv Dror, says there’s something else keeping this market stagnant. “Once an app becomes significant enough to pose a threat to the big players, they either get acquired or significantly handicapped by a competitive feature or restricted access,” he told me via email. He cites Meerkat, a huge 2015 hit I’d nearly forgotten about, which was one of the originating apps in the now-ubiquitous livestreaming trend. Dror worked at Meerkat until the app was forced to shutter. “On my second day working at Meerkat, Twitter decided to cut off our access to the social graph (since they acquired Periscope), which really hurt us in the long run.”

The bigger networks sometimes prevent the rise of smaller services. But the answer cannot be to just stop creating new social apps. “While I don’t want to discourage people from working on new things … It seems like quite an audacious goal at this point to start as a general use social platform and say you’re gonna be the next Twitter or Facebook,” says Dror. “An app based on audience simply can’t compete from that approach. Instead, Chris Dixon’s ‘Come for the tool, stay for the network’ seems like a better approach. Instagram was a tool for putting filters on photos, that attracted the use case which developed into the network. Houseparty is a tool for group FaceTime. Snapchat was a tool for sending disappearing messages. Eventually it grew into a network, which made their Stories feature work, but it wouldn’t have worked if they started with Stories.”

Hopefully some happy accidents, addictive “tools,” and innovation in the face of sameness will push us into a new social internet. Until then, let’s endure the mild strain over switching from Snapchat to Instagram Stories, and enjoy our three weeks with the next Peach.